Hao ambao waliingia kwa siri ili kuupeleleza uhuru wetu tulio nao katika Kristo ni akina nani? Wagalatia 2:4

Maswali ya Biblia No Comments

Nakusalimu katika jina la Mwokozi wetu Yesu Kristo Karibu  tujifunze maneno ya uzima ya Mwokozi wetu.

Ukisoma vyema hapo utaona maandiko yameorodhesha mambo matatu hapo!,
Sasa ili tunafahamu ni yapi hebu tusome kwa kuanzia juu kidogo.

Wagalatia 2:3 “Lakini Tito aliyekuwa pamoja nami, naye ni Myunani, hakulazimishwa kutahiriwa.

4  BALI KWA AJILI YA NDUGU ZA UONGO WALIOINGIZWA KWA SIRI; AMBAO WALIINGIA KWA SIRI ILI KUUPELELEZA UHURU WETU TULIO NAO KATIKA KRISTO YESU, ILI WATUTIE UTUMWANI;

5  ambao hata saa moja hatukujitia chini yao, ili kwamba kweli ya Injili ikae pamoja nanyi.”

Tutaangalia mambo hayo ni yapi moja baada ya lingine.

1. NDUGU WA UONGO.

Watu wote waliookoka na kumuamini Bwana Yesu wanaitwa ndugu hata leo hii yaani tunaita ni ndugu au familia katika Kristo Yesu.
Sasa katika ndugu hawa wapo walio wa kweli na wauongo. Na ndugu wa kweli ni wale waliookoka kweli kweli kwa kumaanisha wasiotazama/kujiangalia wenyewe, wenye kuwajali na kuwapa kipaumbele/nafasi wengine, wenye kulia kwa ajili ya wengine,wenye kujitoa kwa ajili ya wengine.

Wafilipi 4:21
“Mnisalimie kila mtakatifu katika Kristo Yesu. Ndugu walio pamoja nami wawasalimu. ”
Soma pia

1 Wakorintho 16:2

Na ndugu wa uongo ni hao wanaojiingiza katika kanisa lengo lao sio kumtafuta Kristo. Lengo lao kubwa ni kutafuta mambo yao wenyewe tu kama vile Fedha,Fursa mbali mbali ambazo wanaweza wakazipata au kuzileta katika kanisa kwa manufaa yao wenyewe binafsi.
Wengine wanakuja kuangalia tu na kuchunguza uhuru ulio katika Kristo Yesu, na wengi wao ni Mawakala wa ibilisi na nia yao kubwa ni kuriharibu kundi.
Moja ya watu kama hao ni wale wanaozungumziwa katika kitabu cha Wafilipi  tusome.

Wafilipi 3:17 “Ndugu zangu, mnifuate mimi, mkawatazame wao waendao kwa kuufuata mfano tuliowapa ninyi.

18  Maana wengi huenenda, ambao nimewaambieni mara nyingi habari zao, na sasa nawaambia hata kwa machozi, kuwa ni adui za msalaba wa Kristo;

19  mwisho wao ni uharibifu, mungu wao ni tumbo, utukufu wao u katika fedheha yao, waniao mambo ya duniani.

20  Kwa maana sisi, wenyeji wetu uko mbinguni; kutoka huko tena tunamtazamia Mwokozi, Bwana Yesu Kristo”.

Makundi ya yamna hii yapo katika ngazi zote zikiwemo Wachungaji,manabii,waalimu,waimbaji,mitume,washirika nk.

Ni nyakati za kutisha sana hizi ni wakati wa kuwa makini ndugu yangu.

2. WANAJIINGIZA KWA SIRI.

Ndugu hawa wa uongo wanajiingiza kwa siri sana katika kundi wakichukua ule uhalisia wa ndugu wa kweli katika Kristo kumbe sivyo.
Nia zao na dhamiri zao wanajua ni kipi wanachokifanya.

2Wakorintho 11:13  “Maana watu kama hao ni mitume wa uongo, watendao kazi kwa hila, wanaojigeuza wawe mfano wa mitume wa Kristo.

14  Wala si ajabu. Maana Shetani mwenyewe hujigeuza awe mfano wa malaika wa nuru.

15  Basi si neno kubwa watumishi wake nao wakijigeuza wawe mfano wa watumishi wa haki, ambao mwisho wao utakuwa sawasawa na kazi zao”

Unaona hapo? Wanajigeuza na kuwa kama malaika wa nuru lakini asili yao si watu wa nuruni bali gizani!!.

3.KUPELELEZA UHURU.

Sasa ni uhuru wa namna gani ulio katika Kristo Yesu ambao wanaupata watu waliomwamini Yesu Kristo?

Ni uhuru unaotuweka mbali na  utumwa wa Sheria kama ilivyokuwa katika agano la kale.
Katika Ukristo hatuna sheria ya kula vyakula fulani na vingine tusile vina unajisi la!, maana vyakula havituhudhurishi mbele za Mungu.
Au kushika miandamo ya miezi, Sabato, na sikukuu nk.

Wakolosai 2:16 “Basi, mtu asiwahukumu ninyi katika vyakula au vinywaji, au kwa sababu ya sikukuu au mwandamo wa mwezi, au sabato;

17  mambo hayo ni kivuli cha mambo yajayo; bali mwili ni wa Kristo…

20 Basi ikiwa mlikufa pamoja na Kristo mkayaacha yale mafundisho ya awali ya ulimwengu, kwa nini kujitia chini ya amri, kama wenye kuishi duniani,

21  Msishike, msionje, msiguse;

22  (mambo hayo yote huharibika wakati wa kutumiwa); hali mkifuata maagizo na mafundisho ya wanadamu?

23  Mambo hayo yanaonekana kana kwamba yana hekima, katika namna ya ibada mliyojitungia wenyewe, na katika kunyenyekea, na katika kuutawala mwili kwa ukali; lakini hayafai kitu kwa kuzizuia tamaa za mwili”.

Paulo aliwaonya watakatifu/Wakristo walikuwa Galatia maana kulikuwa na Wayahudi waliokuwa wanajiingiza kwa siri katika kanisa la Kristo si kwa lengo la kumtafuta au kumtumikia Bwana bali kwa lengo la kuwataharisha/kuwatwika mizigo watu waliomuamini Yesu Kristo na kutakaswa dhambi zao kwa kuwashikisha sabato, miandamo ya miezi, kujiepusha na vyakula fulani,kutahiriwa ili wakubaliwe na Bwana nk .

Hivyo hizi ni nyakati za kuwa makini si kila fundisho ama pokeo ni la kulikubaki bali tuzijaribu hizo roho je zimetokana na Kristo??

Maratha.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx1

Kwa Mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *