Amepatwa na haya tangu lini?

Uncategorized, Watoto No Comments

Ipo habari ambayo ni muhimu sana wazazi kuifahamu kuhusiana na maisha ya watoto wao. Watu wengi wanapuuzia maisha ya rohoni ya watoto wao wakidhani kuwa shetani hawezi kuyasogelea, kumbe hawajui ibilisi mpango wake unaanzia tangu kwenye msingi wa maisha ya mwanadamu.

Leo tutaazama kisa hiki kimoja katika maandiko. Utakumbuka mitume walipewa amri na Bwana ya kuponya magonjwa na kutoa mapepo, na kweli walipozunguka katika miji na vijiji walirudisha ripoti nzuri, kuwa hadi mapepo yanawatii, Lakini ulifika wakati, si mapepo yote yaliwatii.

Na sababu tutaisoma katika habari hii, ambayo, kuna walikutana na baba mmoja mwenye mtoto ambaye ana mapepo, na walipojaribu kumtoa walishindwa, baadaye Bwana Yesu akaja, akamuuliza swali moja Yule mzee mwenye mtoto, ambalo nataka sote tulijue tusome;

Marko 9:15 “mara mkutano wote walipomwona walishangaa, wakamwendea mbio, wakamsalimu.

16 Akawauliza, Mnajadiliana nini nao?

17 Mtu mmoja katika mkutano akamjibu, Mwalimu, nimemleta mwanangu kwako, ana pepo bubu;

18 na kila ampagaapo, humbwaga chini, naye hutoka povu na kusaga meno na kukonda; nikasema na wanafunzi wako wamtoe pepo, wasiweze.

19 Akawajibu, akasema, Enyi kizazi kisichoamini, nikae nanyi hata lini? Nichukuliane nanyi hata lini? Mleteni kwangu.

20 Wakamleta kwake; hata alipomwona, mara yule pepo alimtia kifafa; naye akaanguka chini, akagaa-gaa, akitokwa na povu.

21 Akamwuliza babaye, AMEPATWA NA HAYA TANGU LINI? AKASEMA, TANGU UTOTO.

22 Na mara nyingi amemtupa katika moto, na katika maji, amwangamize; lakini ukiweza neno lo lote, utuhurumie, na kutusaidia.

23 Yesu akamwambia, Ukiweza! Yote yawezekana kwake aaminiye.

24 Mara babaye yule kijana akapaza sauti, akasema, Naamini, nisaidie kutokuamini kwangu.

25 Naye Yesu akiona ya kuwa mkutano unakusanyika mbio, akamkemea yule pepo mchafu, akamwambia, Ewe pepo bubu na kiziwi, mimi nakuamuru, mtoke huyu, wala usimwingie tena”.

Angalia swali alilomuuliza, “amepatwa na haya tangu lini”? Baba akasema “tangu utotoni”

Nachotaka uone ni kuwa, shetani anaharibu maisha ya watu tangu utotoni, kijana huyu alitaka kuuliwa na ibilisi tangu utotoni.

Leo hii, mashoga wanaandaliwa na shetani tangu utotoni, wauaji wanaandaliwa tangu utotoni, wachawi na waganga wanaandaliwa tangu utotoni, na ndio maana unaona tabia zisizoelewa kwa mwanao ni kwasababu wakati wewe, umelala, shetani anamfunza huyo mwanao,kwa mapepo yake.

Wewe kama mzazi unapaswa ujue wajibu wako kwa mwanao tangu akiwa chini, usimwache , akakua tu ilimradi, yeye mwenyewe hawezi kujiongoza, unapaswa uwe na ratiba ya kumwombea mwanao/wanao, kama Ayubu alivyokuwa anafanya kwa watoto wake wote tena, hata wakati mwingine kwa kufunga . Unapaswa uwe na ratiba kuwafundisha Neno la Mungu, na misingi ya imani, vilevile unapaswa una na nafasi ya kuwaadhibu pale wanapokosea.

Ukizingatia hayo, utakumkuza mwanao, mbali na ibilisi na mapepo wake wabaya. Kumbuka mtoto hafugwi kama vile mbuzi, mtoto analelewa.  Na malezi ndio uzazi. Usizae tu ilimradi wewe ni kidume, una idadi kubwa ya watoto duniani, zaa ukijua kuwa mtoto ni lazima afuatiliwe mienendo yake hatua kwa hatua, ili ajapokuwa mzima awe na kitu cha kuisaidia jamii imjue Mungu.

Hizi ni siku za mwisho, jali maisha ya kiroho ya mwanao. Kwasababu usipotimiza wajibu huo Mungu atakuuliza siku ile.

Bwana akubariki.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *