JE KUNA MAJINI WAZURI?

Maswali ya Biblia No Comments

Katika swali hili tutatazama baadhi ya vipengele ambavyo vitatusaidia kuelewa ujumbe huu vizuri

  1. Je kuna majini wazuri
  2. Je namba za majini ni zipi
  3. Je kuna Pete za majini
  4. Je kuna njia yoyote ya muoata utajiri kwa haraka Kabla ya kuendelea tuelewe kwanza nini maana ya Majini

Majini Ni roho zilizoasi mbinguni, ambazo zilitupwa duniani au kwa jina lingine wanajulikana kama mapepo , ambao walitupwa pamoja na kiongozi wao rusifa (shetani), shetani
Kabla hajaasi alikuwa malaika mzuri sana malaika kitengo cha sifa, lakini kwa kutaka kwake kuwa kama Mungu, ndiko kukamfanya ashushwe chini hadi hivi leo, na jambo hili la kumuasi Mungu hakulifanya peke yake alikwenda pia kuwashawishi malaika ili nao wamuasi Mungu baadhi walikubali na wengine walikataa, waliokubali idadi yao ilikuwa theruthi yaani robo tatu ya malaika huko mbinguni waliokubali kufatana na uongo wa shetani

Baada ya kukubali ilitokea vita mbinguni ambayo ilikuwa kati ya malaika waliokataa na walioasi, baada ya malaika hawa kushindwa (walioasi) adhabu yao ilikuwa kutupwa chini, ndiyo haya majini ambayo kwa jina lingine mapepo yalitupwa hapa duniani

Ufunuo wa Yohana 12:7-9
[7]Kulikuwa na vita mbinguni; Mikaeli na malaika zake wakapigana na yule joka, yule joka naye akapigana nao pamoja na malaika zake;

[8]nao hawakushinda, wala mahali pao hapakuonekana tena mbinguni.

[9]Yule joka akatupwa, yule mkubwa, nyoka wa zamani, aitwaye Ibilisi na Shetani, audanganyaye ulimwengu wote; akatupwa hata nchi, na malaika zake wakatupwa pamoja naye.

Kumbuka pia baada ya kutupwa chini, si kwamba Mungu aliwaondolea nguvu zao, hapana walibaki nazo, ndivyo Mungu alivyo mtu yoyote anapoasi hata kama alikuwa na kipawa au karama kiasi gani Mungu haitoi kwake, anamuachia ndipo hapo sasa inaanza kutumika kinyume na mapenzi ya Mungu, kwa sababu Roho wa Mungu anakuwa hayupo katika ya mtu huyo.

Lakini si kwamba majini (mapepo) yanazo nguvu ya kutushinda sisi tuliokoka hapana hawana nguvu hizo kabisa
Neno la Mungu linasema
“Yesu alipaa juu akateka mateka akatupa vipawa “
Pia
“tumepewa mamlaka ya kukanyanga ng’e na nyoka”

hayo yote yanatuonyesha sisi tunazo nguvu kuliko hayo mapepo.. kwa sababu tuliye naye ndani Yetu Yesu Kristo ni mkuu kuliko hayo mapepo

Baaada ya kujua maana halisi, basi tutazame hivyo vipengele vitakavyo tusaidia kumshinda shetani na Uongo wake

JE KUNA MAJINI WAZURI?

Majini wote ni wabaya hakuna jini hata mmoja aliye mzuri. Shetani aliye mkuu wa majini hayo anatumia nguvu kubwa kuwadanganya watu kwamba kuna majini wazuri..lengo lake ni ili watu wajishughulishe kuzitafuta roho hizo na kujishikamanisha nazo. Na kwa pamoja wafanye kazi ya kuziangusha roho nyingine.

JE PETE ZA MAJINI NI ZIPI?

Majini yanaweza kumwingia mtu yoyote kwa kupitia njia yoyote ile ambayo ipo kinyume na mapenzi ya Mungu sio pete tu!..Majini/mapepo yanaweza kumwingia mtu kwa kupitia mawigi ya kichwani, kwa kupita vipodozi, wanja, kwa kujichora tattoo,kwa kufanya ibada za sanamu na pia njia kuu ni kwa kupita kufanya uasherati na mtu ambaye si mke wako au mume wako na pia kwa kuangalia picha za ngono. Pete inaweza kuwa ni njia ya mwisho kabisa ya kuingiza majini ndani ya mtu.

Mtu anapokwenda kwa mganga au anapojiunga na kikundi fulani cha kichawi kama freemason na vingine anaweza kukabidhiwa pete, mkufu, picha au chochote kile…vitu hivyo ni mlango pia wa kuingiza roho za majini ndani ya mtu.

JE NAMBA ZA MAJINI NI ZIPI?

Maelfu ya watu wasio na ufahamu wanazunguka mitandaoni kutafuta namba za majini..Majini ni roho! hayawezi kuwa na namba za simu za mkononi. Mawakala wao ambao ni waganga wa kienyeji na wachawi ndio wenye namba za simu lakini si mapepo. Hayo ni maroho yanafanya kazi katika ulimwengu wa roho…

JE KUNA NJIA YOYOTE YA KUPATA UTAJIRI WA HARAKA KUPITIA MAJINI?

Uongo mkubwa shetani anaowadanganya wengi ni kwamba kwake kuna fedha za bure na za haraka!..Nataka nikuambie ndugu hicho kitu hakipo..lengo la shetani ni kukupeleka tu kuzimu hakuna lingine.

Njia ifuatayo ndiyo anayoitumia shetani kuwapatia watu mali kwa njia ya majini.

1.Anatumia mtu jini/pepo..Lile pepo linaweza kuwa la aina yoyote ile, aidha zinaa, ulevi, wizi, uuaji n.k Sasa lile jini, tuchukue mfano la zinaa linapomwingia mtu..au mtu anapokwenda kwa waganga kutafuta mali anapewa pete..Na ile pete ndani yake imebeba mojawapo ya hilo jini..labda tuseme la zinaa..Mtu anapoivaa lile pepo la zinaa linamwingia..yule mtu akitoka pale anakuwa mwasherati kupita kawaida…kama ni mwanamke anakuwa ni kahaba kupita kawaida…na hivyo linamsukuma kwenda kufanya kazi ya ukahaba. Na kwa kupitia hiyo kazi ya ukahaba ndipo anapopata fedha.. Lakini si kwamba anakaa tu na kisha fedha zinaingia.

Kadhalika na wizi, ni hivyo hivyo..pepo la wizi linamwingia na linakwenda kumfanya kuwa mwizi hodari..na kwa wizi ule anapata mali zisizohalali.

Na hivyo hivyo mauaji..Pepo linamwingia mtu na kumfanya aone kuua sio shida tena na kwa kupitia mauaji yale anapata kazi nyingi za ujambazi na hivyo kupata fedha kwa kazi hiyo.

Kwahiyo hakuna fedha za bure kwa shetani..Anakupa jini/pepo na jini hilo linakwenda kukutumikisha kupata hizo mali. Na hautakaa tu baada ya kuipokea hiyo pete..kwamba fedha zidondoke.

Hata wale wanaofanya uchawi ujulikanao kama chuma ulete..Nao pia wanavalishwa pepo hilo ambalo linawafanya wateseke kwa hali na mali kufanya uchawi huo..gharama wanazotumia kufanya uchawi huo ni mkubwa kuliko hata faida wanazozipata huko.

Hivyo kuyatafuta majini au kujishughulisha nao ni kujitesa na ni kwenda kinyume na mpango wa Mungu…Kufanya kazi na majini/mapepo ni kuwa Adui wa Mungu rasmi asilimia 100. Na kujitengenezea daraja zuri la kuwa miongoni mwa watakaoteswa sana katika ziwa la moto baada ya hukumu.

Na madhara ya kuwa na majini ni mauti..Majambazi wote kama Neema ya Kristo haitawapitia wanaishia kupigwa risasi, makahaba wote kama Neema ya Kristo haitawafikia wanaishia kufa kwa magonjwa…vivyo hivyo wezi wanaishia kuchomwa moto..Mafisadi wanaishia kufungwa..wachawi wanaishia kufa kifo cha ghafla n.k

Sasa kwanini kudanganyika na uwongo wa shetani kwamba kwake kuna fedha za bure?..Kwamba ni kuvaa pete tu, ni kuchinja mbuzi tu!..shetani anakuambia ni kuvaa pete tu lakini hakuambii ukahaba atakaokwenda kukutumikisha nao.

Hivyo kama Kama hujampa Kristo maisha yako. Mgeukie Leo..usitafute mali wala msaada kwa shetani na wala hakuna majini wazuri watakaokusaidia kupunguza ugumu wa maisha..shetani yeye kashaasi, anachokisubiria tu ni kutupwa katika ziwa la moto..na anataka kwenda na wengi..hivyo anatumia uongo wa kila namna kujaribu kuvuta watu kwake..tumwache aende yeye peke yake sisi tumgeukie Kristo tumaini la utukufu.

Bwana akubariki sana.

NURU YA UPENDO” Kwa kubofya hapa>> WhatsApp: https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema
Kwa msaada pia wasiliana nasi kwa namba hizi

+225693036618/ +225789001312

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *