JE! UMEIAMINI INJILI IPI?

Biblia kwa kina, Uncategorized No Comments


Biblia inasema katika..

Marko 1:15 akisema, Wakati umetimia, na ufalme wa Mungu umekaribia; tubuni, na kuiamini Injili.

Bwana katika maneno hayo alikuwa anatoa taarifa na maelekezo ya nini cha kufanya, na taarifa aliyoitoa hapo ni kuwa, ufalme wa Mungu umekaribia, na maelekezo ya kufanya ni tutubu na kuiamini injili, sasa hadi hapo utakua umeshagundua kuwa, ufalme wa Mungu utakapo kuja (maana upo karibu), hautakua kwaajili ya watu wote, bali ni kwa ajili ya wale watakao tubu dhambi zao na kuiamini injili, ikiwa na maana kwamba, kutubu tu peke yake haitoshi bali unahitaji pia na kuiamini injili, lakini swali ni je! wewe kama mtu uliyetubu Umeiamini injili ipi? Kwa sababu duniani kuna injili zaidi ya moja zinazohubiriwa, tunaweza lithibitisha hilo katika

2 Wakorinto 11:4 Maana yeye ajaye akihubiri Yesu mwingine ambaye sisi hatukumhubiri, au mkipokea roho nyingine msiyoipokea, AU INJILI NYINGINE msiyoikubali, mnatenda vema kuvumiliana naye! 

Umeona hiyo injili nyingine tofauti na injili ya kweli? Hivyo basi, Ikiwa wewe umetubu lakini bado hujaiamini injili sahihi ya BWANA iliyohubiriwa na mitume wake, basi tambua ufalme wa Mungu utakapokuja hautokuhusu, au kama umetubu na hutaki kuiamini injili ya BWANA YESU basi fahamu kuwa, ufalme huu utakapokuja hautokuhusu, bali wale walio tubu na kuiamini injili ya Bwana tu na si vinginevyo

Sasa labda unaweza jiuliza, injili ya Bwana ni ipi? Au ni in ya namna gani? Jibu ni kwamba, Injili ya Bwana ni kumwamini yeye na kisha kubatizwa katika ubatizo sahihi ambao ni wa maji mengi na kwa JINA LA YESU KRISTO sawa sawa na (Matendo 8:16), (Matendo 10:48), kama ulibatizwa vinginevyo ulidanganywa, hiyo siyo injili ya Bwana hivyo rekebisha mapema.


Injili ya Bwana inatutaka kama watu tuliomwamini Kristo, tushiriki meza ya Bwana kwa ajili ya ukumbusho wake hadi atakapokuja. Usiku ule Bwana aliutwaa mkate na kuwapa wanafunzi wake, na wakati anafanya hicho kitendo, mtume paulo hakuwepo lakini utaona baadae baada ya Bwana kupaa, Paulo anakuja kufunuliwa kitu kitu hicho hicho tena

1 Wakorinto 11:23 Kwa maana mimi nalipokea kwa Bwana niliyowapa nanyi, ya kuwa Bwana Yesu usiku ule aliotolewa alitwaa mkate,

24 naye akiisha kushukuru akaumega, akasema, Huu ndio mwili wangu ulio kwa ajili yenu; fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu.

Unaona hapo? Ni kitu kile kile Bwana anakifunua tena kwa mtume Paulo, Sasa hii ni kuonesha kuwa maagizo yake ni yale yale, na endapo umeamini injili nyingine tofauti na hiyo, basi umedanganywa.

Injili ya Bwana pia inatuagiza kutawadhana miguu (yohana 13:3-17 ), na wakati Bwana anatoa haya maagizo mtume Paulo hakuwepo, lakini kitu hicho hicho utakikuta tena kwa Paulo miaka mingi baada ya Bwana kupaa

1 Timotheo 5:10 naye ameshuhudiwa kwa matendo mema; ikiwa amelea watoto, ikiwa amekaribisha wageni, ikiwa amewaosha watakatifu miguu, ikiwa amewasaidia wateswao, ikiwa amefuata kwa bidii kila tendo jema.

Hii ni kuonesha kuwa, maagizo ya Bwana ni thabiti, kama wewe bado hujaamini hili umedanganywa, hiyo ni injili nyingine.

Injili ya Bwana inasisitiza upendo kati yetu na kuwapenda adui zetu

Luka 6:27 Lakini nawaambia ninyi mnaosikia, Wapendeni adui zenu, watendeeni mema wale ambao wawachukia ninyi

Lakini wewe kutwa kumsengenya jirani yako na kuwachukia adui zako, Kama bado upo hivyo jua kua bado hujaiamini injili ya BWANA na ufalme utakapokuj hautokuhusu

Injili ya Bwana inatukataza kuacha wake zetu na waume zetu kwa sababu zetu binafsi

Marko 10:11 Akawaambia, Kila mtu atakayemwacha mkewe na kuoa mwingine azini juu yake;

12 na mke, akimwacha mumewe na kuolewa na mtu mwingine, azini.

Na wazinzi wote hawana urithi katika ufalme wa Mungu (1 Wakorintho 6:9-10), kama wewe umemwacha mke wako au mume wako ni heri upatane naye manake ufalme wa Mungu utakapokuja hautokuhusu.

Injili ya Bwma inaagiza wanawake wajipambe kwa mavazi ya kujisitiri

1 Timotheo 2:9 Vivyo hivyo wanawake na wajipambe kwa mavazi ya kujisitiri, pamoja na adabu nzuri, na moyo wa kiasi; si kwa kusuka nywele, wala kwa dhahabu na lulu, wala kwa nguo za thamani;

Lakini wewe dada unayesema umemwamini Bwana unavaa vimini na suruali ambazo hazilusitiri mwili wako, make up, kope na nywele bandia, kusuka nywele, rasta na kujichubua, ndugu, bado hujaiamini injili wewe, hivyo, amua leo kujikana nafsi, kujitwika msalaba wako na kumfuata Kristo na injili yake

Bwana akubariki, Shalom.