Praitorio ni nini? Na Kwanini ilikuwa ni najisi kwa wayahudi kuingia humo? (Yohana 18:28)

Maswali ya Biblia, Uncategorized No Comments

JIBU… Embu tusome

Yohana 18:28  “Kisha wakamchukua Yesu kutoka kwa Kayafa mpaka Praitorio, nayo ikawa alfajiri; lakini wao wenyewe hawakuingia ndani ya ile praitorio,wasije wakanajisika,bali wapate kuila Pasaka”.

Ukumbi wa hukumu ambao ndio Praitoria,ambao unakuwepo ndani ya majumba ya wafalme, wahalifu wenye kesi ambazo zilipaswa ziamuliwe na Mfalme ..

au liwaji wa mji, basi walipelekwa katika ukumbi huo na kukutana na mkuu huyo na kuhojiwa na moja kwa moja kutolewa hukumu.

Kipindi Wakuu wa makuhani wamemkamata Bwana Yesu, hawakuweza wao wenyewe kumhukumu kwasababu nchi ya Israeli yote ilikuwa chini ya utawala wa Warumi (kwaufupi ilikuwa ni koloni la Warumi)

waliokuwa wanaiongoza serikali yote ni Warumi, na ndio waliokuwa wananatoa hukumu ya mwisho, ndio maana ikawabidi wakuu wa makuhani wampeleka Bwana Yesu kwa Pilato ambaye ndiye aliyekuwa liwali wa Uyahudi, na ndiye mwenye kutoa maamuzi ya mwisho (Mathayo 27:2).

Sasa kwasababu sheria za Wayahudi hazikuwawaruhusu wao kuchangamana na watu wa mataifa, wala kuingia katika nyumba zao tena hususani wakati wa sikukuu, hiyo ikawafanya wale wakuu wa makuhani wabaki nje wakati Kristo anaingizwa ndani ya Praitorio kuzungumza na Pilato.

Wayahudi hawakuingia katika nyumba za watu wa mataifa, kwasababu katika nyumba hizo kulikuwa na vitu najisi vilivyo kinyume na sheria za Musa, mfano wa vitu hivyo ni sanamu, utakuta hata kikombe tu cha kunywea maji kimetengenezwa kwa taswira ya miungu yao, na Zaidi sana vyakula vya watu wa mataifa vingi vilikuwa ni najisi kulingana na sheria za kiyahudi.

Kwahiyo endapo Myahudi akiingia katika nyumba hizo na kushiriki vitu vyao hivyo hata kwa bahati mbaya au kwa kutokujua, basi tayari anakuwa amejitia unajisi, na mtu akiwa najisi anakuwa hastahili kushiriki sikukuu yoyote ya kiyahudi, (anatengwa kwa muda Fulani mpaka unajisi wake utakapoisha)..

Ndio maana ikawepo sheria ya wao kutochangamana na watu wa mataifa wala kuingia katika nyumba zao..utazidi kulithibitisha hilo zaidi kipindi kile Mtume Petro ameenda nyumbani kwa Kornelio..

Matendo 10:26 “Lakini Petro akamwinua, akasema, Simama, mimi nami ni mwanadamu.

27  Na katika kusema naye akaingia ndani, akaona watu wengi wamekusanyika.

28  Akawaambia, NINYI MNAJUA YA KUWA SI HALALI MTU ALIYE MYAHUDI ASHIKAMANE NA MTU ALIYE WA TAIFA LINGINE WALA KUMWENDEA, lakini Mungu amenionya, nisimwite mtu awaye yote mchafu wala najisi.

29  Kwa sababu hiyo nalikuja nilipoitwa, nisikatae; basi nawauliza, ni neno gani mliloniitia?”

Lakini swali ni je! Hiyo sheria ya wayahudi kutochangamana na watu wa mataifa mpaka leo hii ni agizo la Mungu?..Kwamba watu wa mataifa ni najisi mpaka leo??

Jibu ni La!.. Kupitia msalaba wa Yesu Kristo umetufanya wote wawili kuwa mamoja.. Hakuna Myahudi wala Myunani, kwa kumwamini Yesu Kristo sote tunakuwa safi, na kitu kimoja mbele za Mungu, wala hakuna aliye bora kuliko mwingine..yeye Kristo ndiye aliyekibomoa hicho kiambaza cha kati kilichotutenganisha.

Waefeso 2:11  “Kwa ajili ya hayo kumbukeni ya kwamba zamani ninyi, mlio watu wa Mataifa kwa jinsi ya mwili, mnaoitwa Wasiotahiriwa na wale wanaoitwa Waliotahiriwa, yaani, tohara ya mwilini iliyofanyika kwa mikono;

12  kwamba zamani zile mlikuwa hamna Kristo, mmefarakana na jamii ya Israeli, wageni wasio wa maagano ya ahadi ile. Mlikuwa hamna tumaini, hamna Mungu duniani.

13  Lakini sasa, katika Kristo Yesu, ninyi mliokuwa mbali hapo kwanza mmekuwa karibu kwa damu yake Kristo.

14  Kwa maana yeye ndiye amani yetu, aliyetufanya sisi sote tuliokuwa wawili kuwa mmoja; akakibomoa kiambaza cha kati kilichotutenga.

15  Naye akiisha kuuondoa ule uadui kwa mwili wake; ndiyo sheria ya amri zilizo katika maagizo; ili afanye hao wawili kuwa mtu mpya mmoja ndani ya nafsi yake; akafanya amani.

16  Akawapatanisha wote wawili na Mungu katika mwili mmoja, kwa njia ya msalaba, akiisha kuufisha ule uadui kwa huo msalaba.

17  Akaja akahubiri amani kwenu ninyi mliokuwa mbali, na amani kwao wale waliokuwa karibu.

18  Kwa maana kwa yeye sisi sote tumepata njia ya kumkaribia Baba katika Roho mmoja”.

Tunakuwa Najisi tu tunapokuwa nje ya Yesu Kristo, na kinachotufanya kuwa najisi si kitu kingine Zaidi ya dhambi ndani ya maisha yetu, kama Bwana Yesu alivyosema katika Mathayo 15:17-20.

Je! umeokoka?, kama bado unasubiri nini?..Hizi ni siku za mwisho, na Bwana yupo mlangoni.

Ufunuo 22:12 “Tazama, naja upesi, na ujira wangu u pamoja nami, kumlipa kila mtu kama kazi yake ilivyo”

Maran atha!

Jiunge na channel hii kwa Mafundisho zaidi,

NURU YA UPENDO” Kwa kubofya hapa>> WhatsApp: https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini auPiga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *