Arabuni maana yake ni nini? ( Waefeso 1:14)

  Maswali ya Biblia, Uncategorized

Tofauti na mahali/eneo linaloitwa Arabuni, ambalo limetajwa sehemu kadha wa kadha katika biblia, kwamfano ukisoma vifungu hivi utaliona..

Yeremia 25:24 “na wafalme wote wa Arabuni, na wafalme wote wa watu waliochanganyika wakaao jangwani”;

Ezekieli 27:20 “Dedani alikuwa mchuuzi wako, kwa nguo za thamani za kutandikia farasi.

21 Arabuni, na wakuu wote wa Kedari, ndio waliokuwa wafanya biashara wa mkono wako; kwa wana-kondoo, na kondoo waume, na mbuzi; kwa hao walifanya biashara nawe”.

Wagalatia 1:17 “wala sikupanda kwenda Yerusalemu kwa hao waliokuwa mitume kabla yangu; bali nalikwenda zangu Arabuni, kisha nikarudi tena Dameski’.

Ni sehemu ya nchi ambayo ipo mashariki ya kati.

Lakini Neno hili ARABUNI limetumika kuwakilisha jambo lingine tofauti kabisa..

Na jambo lenyewe ni “Hakikisho” au “Garantii” au “Kuponi”

Pale Mungu alipotupa ahadi za uzima wa milele, hakutuacha hivi hivi tu bila hakikisho lake. Yaani alitupa jambo la kutuhakikishia kuwa wokovu huo na uzima huo tumeupata kweli kweli na hivyo tunastahili kuurithi uzima wa milele siku ile.

Sasa hakikisho hilo au garantii hiyo ndio ROHO MTAKATIFU. Hivyo Roho Mtakatifu ndio arabuni yetu.

Kwamfano ukisoma vifungu hivi utaelewa vema..

Waefeso 1:13 “Nanyi pia katika huyo mmekwisha kulisikia neno la kweli, habari njema za wokovu wenu; tena mmekwisha kumwamini yeye, na kutiwa muhuri na Roho yule wa ahadi aliye Mtakatifu.

14 Ndiye aliye arabuni ya urithi wetu, ili kuleta ukombozi wa milki yake, kuwa sifa ya utukufu wake”.

2Wakorintho 1:21 “Basi Yeye atufanyaye imara pamoja nanyi katika Kristo, na kututia mafuta, ni Mungu,

22 naye ndiye aliyetutia muhuri akatupa arabuni ya Roho mioyoni mwetu”.

Hivyo, Roho Mtakatifu akishakuja juu ya Maisha yako, basi ujue, tayari umepokea Garantii ya kuurithi uzima wa milele. Lakini kinyume chake ni kweli usipokuwa na Roho Mtakatifu, hakikisho hilo hauna kwasababu biblia inasema..

Warumi 8:9b “…. Lakini mtu awaye yote asipokuwa na Roho wa Kristo, huyo si wake”.

Sasa swali ni Je! Tunapokeaje Roho Mtakatifu?

Tunapokea Roho kwanza kwa kutubu kwa kumaanisha kabisa kuacha dhambi zetu na kujitwika misalaba yetu na kumfuata Kristo, na baada ya hapo kuwa tayari kubatizwa katika ubatizo sahihi wa kuzamishwa katika maji mengi na kwa jina la Yesu Kristo. Na kisha baada ya hapo ndipo Roho atakaposhuka ndani yako, kukaa nawe milele, hadi siku ile ya ukombozi itakapofika, tutakapokwenda mbinguni kwa tukio lile la unyakuo.

Hivyo ndugu yangu unasubiri nini, hadi sasa huna arabuni ya Roho? Kumbuka siku yoyote ni parapanda, na wafu watafufuliwa, hivyo tubu umgeukie Kristo akuoshe dhambi zako, uwe kiumbe kipya, na Bwana atakupokea..

Ikiwa upo tayari kuokoka leo, au kubatizwa, basi fungua hapa kwa mwongozo wa sala ya toba >>>> SALA YA TOBA

Au tupigie simu kwa namba zetu hizi kwa mwongozo. +255652274252/ +255693036618

Bwana akubariki.

Shalom.

Mada Nyinginezo:

Ufisadi ni nini katika maandiko?(Waefeso 5:18)

Kwanini Ibrahimu alihesabiwa haki na Mungu kabla ya kutahiriwa?

Koga ni nini katika biblia?

Mwezi wa Abibu ni mwezi gani?

LEAVE A COMMENT