USITUMAINIE HEKALU LA BWANA

Shalom, jina la Bwana libarikiwe! Karibu tule chakula cha uzima.

Biblia inasema katika Yeremia 7:4

Yeremia 7:4 Msitumainie maneno ya uongo, mkisema, HEKALU LA BWANA, HEKALU LA BWANA, HEKALU LA BWANA ndiyo haya. 

Nabii Yeremia aliyanena maneno hayo  wakati ambapo wana wa Yuda walipokuwa wakipewa onyo juu ya kwenda utumwani Babeli kutokana kuziacha Amri, sheria, na hukumu za Mungu walizopewa. Ijapokuwa walikuwa wakipewa hayo maonyo, lakini wao hawakujali, waliendelea na njia zao mbaya na tena kuzidi hata watu wa mataifa waliokuwa wamewazunguka.

Ezekieli 5:5 Bwana MUNGU asema hivi; Huu ndio Yerusalemu; nimeuweka kati ya mataifa, na nchi zauzunguka pande zote.

6 Nao umeasi hukumu zangu, KWA KUTENDA MABAYA KULIKO MATAIFA HAYO, nao umeasi sheria kuliko nchi hizo ziuzungukazo; maana wamezikataa hukumu zangu, wala hawakuenda katika sheria zangu.

Lakini, wakati maonyo hayo yalipokuwa yakitolewa, walitokea manabii wa uongo wakiwaambia watu “AMANI AMANI, HAYO  YOTE HAYATOWATOKEA MAANA YERUSALEMU NI MJI WA MUNGU, NA HEKALU LAKE LIMO NDANI YAKE” na huku wanaziacha sheria za Bwana 

Mahubiri haya, yaliwafanya watu kuridhika, na zaidi wakaendelea katika maovu yao huku wakilitumainia HEKALU LA BWANA, Ndipo Yeremia akawaambia msiseme hekalu la Bwana tunalo, HEKALU LA BWANA NDIO HAYA! Haya ninayowaeleza kwa habari ya njia zenu ndio hekalu, Yale YALIYOANDIKWA ndio hekalu la Bwana, na ndio maana lilitangulia Neno la Bwana kwanza ndipo likajengwa hekalu, hivyo, ikiwa hamna kweli ndani ya hilo hekalu, mbele za Mungu ni sawa na nyumba ya sanamu.

Watu hawa waliliacha neno la Bwana (sheria na hukumu zake) kwa maneno ya uongo (mapokeo) huku wakitumaini uwepo wa hekalu utawapa haki kuwa ni watakatifu kwa Bwana. Sasa jambo hili la kujihesabia haki kutokana mapokeo fulani,  au kitu fulani, liliendelea hata wakati wa Bwana Yesu pale alipokuta watu kama hawa (Mafarisayo, Masadukayo na Wasamaria)

Hebu tusome kisa cha msamaria mmoja aliyejihesabia haki kutokana na mapokeo yao……

Yohana 4:19 Yule mwanamke akamwambia, Bwana, naona ya kuwa u nabii!

20 BABA ZETU WALIABUDU KATIKA MLIMA HUU, nanyi husema ya kwamba huko Yerusalemu ni mahali patupasapo kuabudia.

Unaona hapo kwenye mstari wa 20 huyo mwanamke anavyojihesabia haki? akiona kwa jicho la kimwili kwamba, Bwana anaabudiwa  katika mlima Gerizimu ambako baraka zilisomwa na Yoshua (Samaria)?  tofauti wayahudi (mafarisayo na masadukayo) wanavyo dai kuwa ni Yerusalemu?

Sasa unaweza kusema kwa nini huyu mwanamke alisema hivyo?  Historia ya wasamaria ni ndefu kuieleza hapa, hivyo, ukipenda somo lake kwanini waliabudu katika huo mlima unaweza tuandikia ujumbe kwa +255652274252 au +255789001312 ili utumiwe somo lake.

Lakini nachotaka uone hapo ni jibu la Bwana Yesu kwa huyo Msamaria..

Yohana 4:21 Yesu akamwambia, Mama, unisadiki, saa inakuja ambayo HAMTAMWABUDU BABA KATIKA MLIMA HUU, WALA KULE YERUSALEMU.

22 NINYI MNAABUDU MSICHOKIJUA; sisi tunaabudu tukijuacho; kwa kuwa wokovu watoka kwa Wayahudi.

Kwanza Bwana alianza kumjibu kwa kuyakosoa mawazo yao wote, yaani wasamaria wasemao Mlima Gerizimu ni Mlima wa Bwana, na Wayahudi wasemao Hekalu la Bwana, hekalu la Bwana. Kisha akawaambia wasamaria, ninyi mnaabudu msichokijua. Sasa hebu jaribu kutafakari, kwa takribani muda wa miaka 721 hadi wakati wa Yesu kuja duniani wasamaria walikuwa wakiabudu WASICHOKIJUA? Jibu ni ndio! Na hii yote ni kutokana na mahubiri ya mapokeo yao waliyoyapokea kutoka kwa wazee wao na kukataa neno la Mungu. 

Je! mapokeo haya hayapo na kwetu pia?Hatuna watu wasemao hekalu la Bwana, Hekalu la Bwana yaani KANISA la Bwana (mitume);  KANISA LA BWANA, AU DHEHEBU LA KWANZA? usipomwamini nabii huyu hutaenda mbinguni? Je! Hatuna watu wasemao dhehebu letu ndio kongwe tena tajiri? Lakini ukiiwauliza kwa habari ya neno wanasema Mungu anaangalia matendo?(wakizani Mungu anangalia matendo yao mazuri tu sio yale mabaya) Biblia imekuwa si kitu kwao bali mapokeo ya wanadamu na hofu waliyonayo kwa Mungu ni mafundisho ya wanadamu.

Isaya 29:13 Bwana akanena, Kwa kuwa watu hawa hunikaribia na kuniheshimu kwa vinywa vyao, bali mioyo yao wamefarakana nami, na kicho chao walicho nacho kwangu ni MAAGIZO YA WANADAMU WALIYOFUNDISWA;

Sasa hayo mafundisho uliyofundishwa na wanadamu unayajua ni yapi? Je! Unadhani hayatumii maandiko? Yanatumia ila yameingizwa kwa werevu mno kama tu yale ya wasamaria, Kama tu yale ya mafarisayo na masadukayo, na hayo mafundisho yanapokomaa ndani ya mtu, huyo mtu hawezi kupokea ufunuo wowote wa Neno la Mungu, bali atabaki kughadhabika tu kila anaposikia kweli inayopingana mafundisho yake.

Jua kuwa, HAKUNA ASEMAYE YESU KRISTO NI BWANA NA MWOKOZI WANGU HALAFU AKACHUKIZWA NA NENO LA KRISTO. Ukijiona upo hivyo ndugu fahamu kuwa, ulichokitukuza wewe kipo kinyume na Neno la Mungu, unamsulubisha Kristo bila kujua kama tu mafarisayo na masadukayo ambao Bwana aliwaambia..

Luka 16:15 Akawaambia, Ninyi ndinyi mnaojidai haki mbele ya wanadamu, lakini MUNGU AWAJUA MIOYO YENU; KWA KUWA LILILOTUKUZWA KWA WANADAMU HUWA CHUKIZO MBELE ZA MUNGU

Pia anakuambia na wewe, Unalolitukuza,  unalojivunia kwa wanadamu ni chukizo kwa Mungu, ndio maana Mungu anatuma watu kwako, lakini wasema mimi nimezaliwa katika dhehebu hili, na  nitakufa dhehebu hili, basi wewe ni farisayo ama sadukayo, ungepata nafasi ya kuwepo wakati ule Yesu anasulubishwa, ungeshiriki kikamilifu kuondoa mtu anayepingana na mapokeo yako. 

Geuka leo umwabudu Mungu katika kweli ya Neno lake(Roho na kweli) sio Dini au Dhehebu au Nabii au mtume au wafu au sanamu ya mtu. Ukiona unaendelea kuguswa na injili ya kweli kisha unakasirika, UJUE UNA SHINGO NGUMU, NA MIMI SISEMI UTABADILIKA, maana ni makusudi ya Mungu pia waovu wawepo katika siku ya uovu. 

Mithali 16:4 Bwana amefanya kila kitu kwa kusudi lake; Naam, hata wabaya kwa siku ya ubaya.

Maran atha!

+255755251999


Mada zinginezo:

Je! Ni kweli Mariamu mama yake Bwana Yesu alipalizwa mbinguni?


JE! KUNA TOFAUTI GANI KATI YA MTU WA MUNGU NA MTOTO WA MUNGU?


Ni thawabu gani inayozungumziwa katika (Mathayo 6:16)?


NIFANYE NINI KAMA MKRISTO ILI MUNGU ANIONGEZEE IMANI KWAKE?


KUFANYA MATENDO MEMA HAIMAANISHI KUWA UMESHAUPATA WOKOVU

3 thoughts on - USITUMAINIE HEKALU LA BWANA
  1. tukisoma kitabu cha ufunuo 13:8 kinasema watu wote wasio andikwa katika kitabu cha uhai cha mwanakondoo watamwabudu mnyama, swali ni kwamba ni kwanamna gani watu hao wanamwabudu mnyama?

  2. Watu watamwabudu mnyama kwa kukubaliana na mifumo atakatoileta ama kuianzisha watu wengi watakubaliana nayo na hiyo mifungo ama sera atakazozianzisha atapata kubali kwa watu wengi watamsapoti na kukubaliana nae katika kila jambo.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *