Bwana Yesu si Mungu mweza yote (Baba) kulingana na Yohana 14:28?

Yohana 14:28  Mlisikia ya kwamba mimi naliwaambia, Naenda zangu, tena naja kwenu. Kama mngalinipenda, mngalifurahi kwa sababu naenda kwa Baba, KWA MAANA BABA NI  MKUU  KULIKO MIMI. 

Shalom, watu wengi leo hii kwa kukosa ufunuo wa maandiko kwa msaada wa Roho mtakatifu wameshindwa kumwelewa Mungu kwa kutaka kutumia hekima zao za kibinadamu kuyathibitisha maneno ya Mungu na wengine kufikia hatua ya kumwita Bwana Yesu ni Yesu na Baba yake ndiye YEHOVA jambo ambalo si sahihi kabisa. Sasa maandiko yanasema hivi katika Zaburi,

Zaburi 25:14  Siri ya Bwana iko kwao wamchao, Naye atawajulisha agano lake. 

Kumbe Mungu ana siri na siri hiyo haipo kwa watu wote bali kwa wale wanaomcha tu na wale ambao Bwana mwenyewe atapenda kuwafunulia mfano Tomaso (Yohana 20:28) na ndio maana paulo kwa kulijua hilo aliandika

1 Timotheo 3:16  Na bila shaka siri ya utauwa ni kuu. Mungu alidhihirishwa katika mwili, Akajulika kuwa na haki katika roho, Akaonekana na malaika, Akahubiriwa katika mataifa, Akaaminiwa katika ulimwengu, Akachukuliwa juu katika utukufu. 

Sasa basi hebu tuangalie Bwana alimaanisha nini kusema Baba ni mkuu kuliko mimi. Kwanza fahamu ukuu unaozungumziwa hapo si ukubwa wa umri bali wa madalaka, mfano mtu anayemtuma mtu mfulani huyo ni mkuu kuliko yule aliyetumwa, hivyo basi Bwana Yesu na yeye alitumia tafsiri hiyo ya kibinadamu ili aeleweka zaidi, chukulia mfano angesema kuwa amejituma, ni wazi asingeeleweka kwa urahisi sana. Sasa Bwana Yesu alitumwa na nani? Jibu tunasoma katika

Luka 4:18  Roho wa Bwana yu juu yangu, Kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, Na vipofu kupata kuona tena, Kuwaacha huru waliosetwa, 

Umeona? Kumbe Alitumwa na Roho wa Bwana na ndio sababu ya yeye kusema kuwa Baba yaani Bwana ni mkuu kuliko mimi kwani alitumwa na Roho wake. Sasa huyu Roho wa Bwana ni Roho wa nani? Kama tulivyosema Siri ya uungu ni kuu mno, Roho wa Bwana ni Roho wa Bwana Yesu huyo huyo

Matendo Ya Mitume 16:7  Walipofika kukabili Misia wakajaribu kuenda Bithinia, lakini Roho wa Yesu hakuwapa ruhusa, 

Unaweza soma tena Wafilipi 1:19    2 Wakorintho 3:17

Sasa kumbe huyu Roho wa Bwana kwa jina lingine ni Roho wa Yesu, hivyo basi huyo Bwana anayezungumziwa hapo ni Yesu mwenyewe umeona hapo? 

Na ndio maana sehemu moja anasema kwamba Roho mtakatifu atapelekwa na Baba na pia sehemu nyingine anasema kuwa yeye atampeleka Roho mtakatifu. 

Yohana 14:26   Lakini huyo Msaidizi, huyo Roho Mtakatifu, ambaye Baba atampeleka kwa jina langu, atawafundisha yote, na kuwakumbusha yote niliyowaambia. 

Harafu soma na 

Yohana 16:7   Lakini mimi nawaambia iliyo kweli; yawafaa ninyi mimi niondoke, kwa maana mimi nisipoondoka, huyo Msaidizi hatakuja kwenu; bali mimi nikienda zangu, nitampeleka kwenu. 

Sasa jiulize swali, Roho mtakatifu anapelekwa na wawili? Jibu ni la! Na mmoja tu ambaye ndiye Baba ambaye ndiye Bwana Yesu mwenyewe, na ndio maana alisema hivi

Yohana 14:7  Kama mngalinijua mimi, mngalimjua na Baba; tangu sasa mnamjua, tena mmemwona. 

Hivyo basi  Bwana Yesu ndiye Mungu mwenyewe na hii siri hata mitume walikuja kuielewa baadae na kuandika hivi

Warumi 9: 5  ambao mababu ni wao, na katika hao alitoka Kristo kwa jinsi ya mwili. Ndiye aliye juu ya mambo yote, Mungu, mwenye kuhimidiwa milele. Amina. 

Na siku moja kila goti litapigwa mbele zake na kila ulimi utamkiri kwamba Yesu ni Mungu. Ndugu yangu, usichukuliwe na mafundisho ya uongo ambayo yanamkana Bwana kwani hayatokani na Mungu. 

Hivyo basi kwa kuhitimisha ni kwamba Bwana Yesu ndiye yeye Mungu mweza yote na tena ni peke yake kama maandiko yanavyothibitisha katika

1 Timotheo 6:14 kwamba uilinde amri hii pasipo mawaa, pasipo lawama, hata kufunuliwa kwake Bwana wetu Yesu Kristo;

15 ambako yeye kwa majira yake atakudhihirisha, yeye aliyehimidiwa, MWENYE UWEZA PEKE YAKE, Mfalme wa wafalme, Bwana wa mabwana;

Bwana akubariki. Shalom


Mada zinginezo:

Je! Ni kweli Bwana Yesu alishika sabato kuninganana luka 4:16?


Jina la BWANA (Mungu) ni Yesu Kristo?


Je! Kuna Mungu wawili? (Kulingana na Yohana 1:1)


Ni Mtume gani aliyekuwa Mkuu na Wa kwanza  kuliko wote katika biblia?


VIFUNGO VYA WOTE VIKALEGEZWA.

2 thoughts on - Bwana Yesu si Mungu mweza yote (Baba) kulingana na Yohana 14:28?
  1. Mimi imani yangu ni ktk Utatu Mtakatifu ie Baba, Mwana na Roho Mtakatifu. Sasa kutokana na fundisho lako ina maana hakuna Utatu, Yesu ni kila kitu? Na pale msalabani Yesu aliposema Mungu wangu,Mungu wangu mbona umeniaacha alikuwa anajisemea mwenyewe? Naomba unisaidie zaidi

  2. Ikiwa Yesu Kristo kwako ndio njia pekee ya kukufikisha mbinguni, wala hakuna mwingine zaidi yake, na kwamba waamini kuwa yeye ndio mwokozi wa ulimwengu. Basi hiyo kwako inatosha kukupa wokovu haijalishi, utamwona kama ni mmoja kati ya watatu.. Hasara utakayopata ni kwamba hujafikia katika utimilifu wote wa kijua siri ya Mungu..ambayo ipo ndani ya Kristo Yesu.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *