Kwa nini mitume wote na manabii mpaka mapapa ni weupe? Je ngozi nyeusi imelaaniwa?

Maswali ya Biblia No Comments

 

Nakusalimu katika Jina la Yesu Kristo.

Mungu wetu Hana Upendeleo (soma kumb 10:17, Rumi 2:11, Galatia 3:28), tusoma haya kwa pamoja..

Matendo ya Mitume 10:34-35
34″ Petro akafumbua kinywa chake, akasema, Hakika natambua ya kuwa Mungu hana upendeleo;

35 bali KATIKA KILA TAIFA MTU AMCHAYE na kutenda haki HUKUBALIWA NA YEYE.”

 

Tangu Uumbaji mpaka Agano la kale Mungu alichagua uzao wa Ibrahim yaani Israel kama taifa ambalo angelitumia kwa kukamilisha mpango wake wa wokovu wa Wanadamu, hivyo Hilo ndilo lililoteuliwa kuwa taifa la Mungu miongoni mwa mataifa yote ulimwenguni.

Mungu hakutumia Rangi kama kigezo Cha kulichagua taifa la Israel, Wala kigezo kingine chochote, angeweza kuchagua mataifa makubwa yaliyokuwa pembezoni mwa Israel Mfano Rumi, ugiriki n.k.

Na pia Waisrael hawakuwa weupe sana, kulinganisha na mataifa mengine yaliyokuwa na rangi hiyo, ukiwaangalia hata Leo utagundua Wana asili Fulani kama waarabu hivi lakini Si wazungu halisi.

Pia taifa hili halikuwa na chochote lilikuwa taifa dhaifu na la kawaida kabisa, lakini Mungu mwenyewe alilichagua kwa kutimiza Mpango wake wa wokovu kupitia Bwana wetu Yesu Kristo.

Biblia yenyewe haijabagua rangi (nyeupe wala Nyeusi) labda mhindi au mzungu, mwarabu kama mtume au nabii wa BWANA, Bali lililotumika ni taifa la Israel pekee.

Yalikuwako mataifa makubwa kipindi hicho kuzidi hata Israel yenyewe lakini hawakuruhusiwa hata kumkaribia Mungu katika masuala ya ibada, ila Israel pekee!

Lakini baada ya kudhihirishwa kwa Bwana Yesu Kristo ulimwenguni sote tumefanyika kuwa sawa mbele za Mungu, hakuna Tena Israel kama taifa la Mungu Bali yeyote amchaye YEYE alimfanya kuwa taifa lake(Yohana 1:12) kupitia Yesu Kristo.

Ndio maana Leo tuna Wachungaji, Waalimu na hata mitume kutoka mataifa mbalimbali tofauti na Israel (Africa yote, china, India n.k).

Hivyo basi ni dhahiri kuwa mtazamo wa kusema kuna ngozi imelaaniwa kuliko nyingine Si sahihi! Maana Mungu Hana Upendeleo. Ingalikuwa hivyo walikuwepo mataifa makubwa yenye rangi nyeupe kipindi Cha Agano la kale lakini alilichagua Israel kama taifa lake, ili watu wamjue kuwa kuna Mungu wa Israel.(ni vyema kufahamu pia Waisrael wote sio weupe bali wapo wengine wenye asili ya weusi ukienda Ethiopia utakuta pia wapo)

Maandiko Matakatifu yanasema…

Waefeso 2:11 “Kwa ajili ya hayo kumbukeni ya kwamba zamani ninyi, mlio watu wa Mataifa kwa jinsi ya mwili, mnaoitwa Wasiotahiriwa na wale wanaoitwa Waliotahiriwa, yaani, tohara ya mwilini iliyofanyika kwa mikono;

12 kwamba zamani zile mlikuwa hamna Kristo, mmefarakana na jamii ya Israeli, wageni wasio wa maagano ya ahadi ile. Mlikuwa hamna tumaini, hamna Mungu duniani.

13 Lakini sasa, katika Kristo Yesu, ninyi mliokuwa mbali hapo kwanza mmekuwa karibu kwa damu yake Kristo.14 Kwa maana yeye ndiye amani yetu, aliyetufanya sisi sote tuliokuwa wawili kuwa mmoja; akakibomoa kiambaza cha kati kilichotutenga.

15 Naye akiisha kuuondoa ule uadui kwa mwili wake; ndiyo sheria ya amri zilizo katika maagizo; ili afanye hao wawili kuwa mtu mpya mmoja ndani ya nafsi yake; akafanya amani.

16 Akawapatanisha wote wawili na Mungu katika mwili mmoja, kwa njia ya msalaba, akiisha kuufisha ule uadui kwa huo msalaba”.

 

Kuhusu masuala ya Upapa, kuanzia mifumo ya uendeshaji na misimamo, Si kama biblia inavyoagiza (mfano ushoga, ibada za wafu, n.k) hivyo hatuwezi kuwaweka kundi moja pamoja na mitume na Manabii.

Ubarikiwe sana.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa Mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *